KIKAO cha Bunge la Bajeti kinaendelea mjini Dodoma huku hoja kadhaa zikiwasilishwa na kutoa nafasi kwa wabunge ambao ndio wawakilishi wa wananchi, kuchangia hoja hizo kwa maslahi mapana ya taifa hili na vizazi vijavyo.
Bunge hili lenye wabunge kutoka vyama vya CCM, CHADEMA, CUF, NCCR, TLP na UDP limekuwa na mvuto wa aina yake likiaminika kuwa lina nafasi ya kufikisha serikalini maoni na mitazamo ya Watanzania wenye itikadi tofauti.
Mvuto wa Bunge hili umeanza kupungua hasa kutokana na namna hoja zinavyowasilishwa, zinavyochangiwa, zinavyoungwa mkono na hata namna zinavyopingwa, ikidaiwa na wengi kuwa yapo makosa makubwa ambayo wabunge wanawafanyia waliowatuma Dodoma.
Matusi na maneno ya kejeli yanayotolewa hata wakati usiostahili ndani ya jumba hilo ‘takatifu’ limekuwa jambo la kawaida kwa wabunge wetu na hata wakikemewe au kuombwa kulinda heshima yao kwa kutumia maneno yenye staha kwa binadamu, hawabadiliki.
Wengi hujiuliza, hivi wabunge hawa ambao wote ni watu wazima wanataka kuonyesha picha gani duniani juu ya jamii yetu? Dunia iamini kuwa jamii inayowakilishwa na wabunge hawa inafanana nao? Jamii yetu haifundishiki? Jamii yetu imeoza kiasi cha kutukana kwenye kipaza sauti?
Ni aibu kubwa sana. Ni aibu kiasi kwamba wapo watu wanaodhani wakati umefika wa kuwatoa watoto sebuleni wakati wakubwa wakiufuatilia mijadala bungeni. Kwanini wabunge wanatupekeka huko? Ni kweli tumeoza kimaadili kiasi hiki!
Inafahamika kuwa si wabunge wote wenye lugha chafu kiasi hicho, lakini hao wachache wanachafuliwa na wenzao. Sasa dunia itaamini kuwa iwapo wawakilishi wa wananchi maadili yao yameporomoka kiasi hiki, basi nchi nzima imeoza.
Hapana, wakati umefika sasa wa wabunge kubadilika. Wavumiliane, waache kujibu tusi kwa tusi; bali iwe tusi kwa hoja. Waache kujibu kejeli kwa kejeli; bali iwe kejeli kwa ukweli. Waache kuwasha mic wakati zamu yao haijafika.
Kama wabunge hawafundishiki hata baada ya semina elekezi wanazopewa na Spika na viongozi wengine, wapiga kura wawaeleweje?
Maoni